NAIBU WAZIRI ANGELINA MABULA AZISHAURI HALMASHAURI ZA MUSOMA KUNUNUA NYUMBA ZA NHC

Naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Angelina mabula akizungumza mara baada ya kukagua mradi wa nyumba za shirika la nyumba la taifa (NHC) wakati wa ziara yake mkoa wa Mara.
……………….
Na Mwandishi Maalum- Mara
Naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi Angelina mabula amezishauri halmashauri  za mji na wilaya ya Musoma mkoa wa Mara kununua nyumba zilizojengwa na  shirika la nyumba la taifa (NHC) kwa ajili ya watumishi wake.
Mabula ametoa ushauri huo alipotembelea nyumba hamsini zilizojengwa na shirika la nyumba la taifa (NHC) katika eneo la Buhare katika manispaa ya  Musoma mkoani Mara.
Amesema, ni jukumu la serikali kuhakikisha watumishi wake wanakuwa na makazi bora na rahisi kwao hasa pale mtumishi anapohitajika kwa haraka katika kutekeleza majukumu yake.
Naibu waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi alisema, alitegemea halmashauri za Musoma zingezichukua nyumba hizo zilizojengwa na shirika la nyumba kama ambavyo imefanyika katika maeneo mengine ya Geita na Uyui.
Amezitaka halmashauri za mji na wilaya ya Musoma kulitumia shirika la nyumba la Taifa (NHC) katika kujenga nyumba zake pamoja na kupanga katika nyumba za shirika hilo.
Aidha, alizitaka halmashauri kuhakikisha zinapeleka huduma muhimu kama maji na miundo mbinu katika maeneo ambayo shirika la nyumba la taifa  linaendesha miradi yake ili kupunguza gharama za ujenzi na hivyo kuleta unafuu wakati wa kuuza nyumba na kupanga.
Naibu Waziri wa Ardhi nyumba na maendeleo ya makazi  ameshauri pia nyumba za shirika hilo ambazo serikali imeshindwa kuzinunua zitangazwe kwa wananchi ili wale wenye uwezo waweze kuzinunua kwani ni nyumba bora na za kisasa.
Naye Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) Frank Mambo, amemueleza Naibu Waziri wa ardhi nyumba na maendeleo ya makazi kuwa mradi wa ujenzi wa nyumba 50 wenye lengo la kuwapatia wananchi makazi bora ulianza mwaka 2014 na unatarajia kukamilika Machi 2018. Amesema mradi huo unahusisha nyumba za makazi, maduka, zahanati na maeneo ya kupumzikia.

Post a Comment

Previous Post Next Post