WAGONJWA 25 WANATARAJIWA KUFANYIWA UPASUAJI WA MOYO WA KUFUNGUA KIFUA KATIKA KAMBI MAALUM YA MATIBABU

Na Mwandishi Maalum
19/3/2018 Jumla ya wagonjwa 25 wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua katika kambi maalum ya matibabu ya siku sita inayofanyika  katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Upasuaji huo unafanywa na madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Taasisi ya Open Heart International (OHI) ya nchini Australia.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi leo jijini Dar es Salaam  Daktari bingwa wa upasuaji wa  moyo na mishipa ya damu ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi wa Kurugenzi ya upasuaji Bashir Nyangasa alisema wagonjwa watakaofanyiwa upasuaji watoto ni  15 na watu wazima 10.
Dkt. Nyangasa alisema kambi hiyo imeenda  sambamba na upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wagonjwa 65 kati ya hao watoto 35 na watu wazima  30. Wagonjwa ambao wamefanyiwa uchunguzi na hawatafanyiwa upasuaji katika kambi hiyo watafanyiwa upasuaji na madaktari wa JKCI.
“Watoto tunaowafanyiwa upasuaji ni wale wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na mishipa ya damu kutopitisha damu  vizuri katika moyo na kwa watu wazima tunapandikiza mishipa ya damu kwenye moyo (CABG – Coronary Artery Bypass Grafting) na kubadilisha milango ya moyo miwili hadi mitatu iliyoziba au haifungi vizuri.
Kabla ya kuanza kwa kambi hiyo kulikuwa na mafunzo ya kiuguzi ya siku tano ya utoaji  huduma bora kwa  wagonjwa wa upasuaji wa moyo  yalitolewa na Taasisi ya Open Heart International kwa  wauguzi 30 wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete.
Hadi sasa wagonjwa wanne wameshafanyiwa upasuaji wa moyo  kati ya hao watoto wawili na watu wazima wawili na hali zao zinaendelea vizuri .

Post a Comment

Previous Post Next Post