DHAHABU KILO 9 ILYOKUWA INATOROSHWA YAKAMATWA JIJINI MBEYA

-Waziri Mavunde aingia mtaani na kikosi kazi kwenye eneo la maficho

-Aupongeza Uongozi wa Mkoa na Vyombo vya Usalama Mbeya

-Aagiza kusimamisha Leseni za biashara ya Madini za watuhumiwa

-Dhahabu iliyokamatwa ina thamani ya Tsh 1,555,476,586

-Serikali ingepata mapato ya Tsh 144,659,322

Jeshi la Polisi Mkoani Mbeya linawashikilia wafanyabiashara wa madini 10 kwa tuhuma za utoroshaji wa madini Kilogramu 9.8 yenye thamani ya Tsh 1,555,476,586.

Akitoa taarifa hiyo kwa wanahabari,Waziri wa Madini Mh. Anthony Mavunde amesema wafanyabiashara hao walikamatwa siku ya Jumamosi saa 10:27 Alfajiri Katika mtaa wa Ilomba Jijini Mbeya  kwenye nyumba waliyokuwa wamepanga wakiwa na vipande 344 ya dhahabu iliyochomwa yenye uzito wa Kilogramu 9.8 pamoja  na vifaa mbalimbali kama vile Precious Metal analayzer (XRF) aina ya Niton DXL thermoscientific, mitungi ya gesi, jiko na vyungu kwa ajili ya kuchomea dhahabu, Kipimo cha maji cha kupimia dhahabu, mizani kadhaa pamoja na kemikali aina ya borax.

Mh Mavunde ameupongeza uongozi wa Mkoa wa Mbeya chini ya Mh. Juma Homera na vyombo vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na Kikosi Kazi cha Wizara ya Madini kufanikisha ukamataji wa watuhumiwa hao.

Waziri Mavunde ametoa rai kwa wafanyabiashara wote wa madini kuhakikisha wanazingatia sheria na kanuni za kufanya biashara ya madini nchini na wote watakaobainika kutorosha madini watachukuliwa hatua za kisheria pamoja na kufutiwa Leseni zao.

Aidha Waziri Mavunde ameagiza kusimamishwa kwa Leseni za biashara ya Madini za watuhumiwa nchi nzima wakati taratibu za upepelezi zikiendelea kabla ya kufikishwa Mahakamani.

Akizungumza katika zoezi hilo,Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya wa Chunya Mh. Mbaraka Batenga amewataka viongozi wote wa mitaa na vijiji kuwatambua watu katika maeneo yao kwa kuwasajili katika daftari la wakazi na kuwataka wamiliki wa nyumba za kupanga kuhakikisha wanawafahamu vyema wapangishaji wao na shughuli zao.

Post a Comment

Previous Post Next Post